Mageuzi ya Umoja wa Mataifa yasikate maendeleo
Katika kipindi hiki ambapo Umoja wa Mataifa unakabiliwa na changamoto za kifedha na mjadala wa mageuzi ya mfumo wake ukiendelea, Balozi Mavura amesema Tanzania inaunga mkono mageuzi yatakayoongeza ufanisi, lakini bila kuathiri programu za maendeleo kwa nchi zinazoendelea.
Amesema mataifa kama Tanzania bado yanahitaji mchango mkubwa wa Umoja wa Mataifa katika maendeleo, hivyo kupungua kwa fedha hakupaswi kuwa sababu ya kupunguza huduma muhimu kwa wananchi.
“Tunataka kuhakikisha kwamba kupungua kwa fedha kisiwe kisingizio cha kukata programu za maendeleo,” amesema.
Amesisitiza umuhimu wa kutafuta uwiano kati ya mageuzi na ufanisi kwa upande mmoja, na kuendelea kusaidia nchi zinazohitaji zaidi msaada wa Umoja wa Mataifa kwa upande mwingine.
Ahadi kwa Watanzania
Akihitimisha mahojiano hayo, Balozi Mavura amewahakikishia Watanzania kwamba ataitumikia nchi kwa weledi, maarifa na kujituma kikamilifu katika jukwaa la Umoja wa Mataifa.
“Watanzania wategemee kama nilivyoapa mbele ya Mheshimiwa Rais, nitawatumikia kwa uwezo wangu wote, weledi wangu wote na maarifa yangu yote kuhakikisha kwamba maslahi yao na maslahi ya nchi yetu yanazingatiwa katika eneo hili ambapo maslahi ya dunia yanatengenezwa.”
