Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Malta zimekubaliana kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Malta zimekubaliana kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia baina yao.
Wawakilishi wa Kudumu wa mataifa hayo mawili katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi wa Tanzania na Christopher Grima wa Malta ndio waliotia sahihi hati za kuridhia kuanzishwa kwa uhusiano huo na ambao utakuwa katika ngazi ya Mabalozi.
Wakizungumza mara baada ya utiaji sahihi hati hizo, wawakilishi hao wameelezea kuwa kuanzishwa kwa uhusiano huo ni hatua muhimu sana katika kukuza na kuendeleza ushirikiano na uhusiano kati ya mataifa hayo mawili na watu wake.
Tanzania imekuwa ikinufaika kwa ufadhili wa nafasi za masomo kutoka Malta kwa watumishi mbalimbali wakiwamo wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Wizara nyingine.


Mhe Jaji Mkuu Mohamed Othman Chande akabidhi ripoti ya jopo lake kwa katibu mkuu
Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon amepokea ripoti ya Jopo huru la wataalamu alilounda kupitia na kuchambua taarifa mpya kuhusu kifo cha Bw. Dag Hammarskjold aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
Kiongozi wa Jopo hilo alikuwa Mhe. Jaji Mkuu wa Tanzania Othman Chande akishirikiana na wanajopo wengine ambao ni Bw. Kerry Macaulay kutoka Australia na Bw. Henrik Larsen wa Denmark.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Katibu Mkuu, inaeleza kwamba, Katibu Mkuu ameipokea taarifa hiyo na kuwashukuru wanajopo hao kwa kazi nzuri na kubwa na kwa mchango wao muhimu katika kutafuta ukweli kuhusu mazingira yaliyosababisha kifo cha Katibu Mkuu wa zamani Dag Hammarskjold pamoja na wajumbe wengine aliokuwa amefuatana nao usiku wa tarehe 17-18 September 1961.
Taarifa hiyo inaeleza zaidi kwamba, Katibu Mkuu, ameridhishwa kwamba jopo hilo liliweza kwenda Zambia na kuzungumza na mashahidi na kwamba jopo limeweza kukusanya nyongeza ya taarifa mpya kutoka kwa nchi wanachama na vyanzo vingine zikiwamo maktaba binfasi huko Belgium, Sweden na Uingereza.
Taarifa ya msemaji wa Katibu Mkuu inaeleza kuwa Katibu Mkuu ataipitia taarifa hiyo kwa umakini mkubwa na kwa haraka na kisha kwa ataiweka ripori hiyo pamoja na uchambuzi wake(Katibu Mkuu) na mwelekeo wa baadaye kwa Nchi Wanachama mapema iwezekanavyo.

Tanzania yashiriki mkutano wa sheria ya bahari

Wanafunzi wa Feza watembelea uwakilishi
